Kama ilivyo desturi kwa mwanamuziki nyota kutoka Barbados anayeishi Marekani, Rihanna ameendelea kutumia matukio maalumu kufichua ujauzito wake. Safari hii, ameonesha ujauzito wake wa tatu katika tukio la kifahari la Met Gala 2025, lililofanyika usiku wa kuamkia leo Mei 6, 2025.
Msanii huyo alithibitisha kuwa yeye na mpenzi wake wa muda mrefu, A$AP Rocky, wanatarajia kupata mtoto wa tatu. Ambapo kwa sasa, wanandoa hao wana watoto wawili wa kiume ambao ni RZA Athelston Mayers na Riot Rose Mayers.
Mwezi mmoja uliopita, Rihanna alivuta hisia za mashabiki mitandaoni kutokana na mavazi yaliyomfunika tumboni, hali iliyozua tetesi kuwa huenda alikuwa mjamzito.
Tetesi hizo sasa zimethibitishwa rasmi kupitia maonesho yake ya Met Gala.
Baada ya Rihanna kuonesha wazi tumbo lake la ujauzito, A$AP Rocky alifunguka kwa furaha na kusema:
“Vazi la Rihanna usiku wa leo... sijui, halifichi sana tumbo lake la ujauzito, unajua? Ni wakati wa kuonyesha ulimwengu kile tulichokuwa tukikipika.”
Hii si mara ya kwanza kwa Rihanna kufichua ujauzito wake katika tukio kubwa. Mwaka 2023, alitangaza ujauzito wake wa pili hadharani wakati wa onyesho la Super Bowl Halftime Show.
Ikumbukwe kuwa mwishoni mwa mwaka 2024, Rihanna alieleza wazi kuwa anatamani kupata mtoto wa kike.
“Sijui Mungu anataka nini, lakini ningependa kuwa na zaidi ya wawili. Ningependa kujaribu kupata binti wangu. Kama tukipata mtoto wa kike, mambo mengi yasiyotegemewa yatajitokeza. Itakuwa hali mpya kabisa.”
Baada ya kuthibitisha ujauzito huo, mashabiki na wafuasi wake wamefurahia hatua hiyo mpya na kumuombea apate kile anachokitamani mtoto wa kike.

Leave a Reply